Nenda kwa yaliyomo

Vita ya Dien Bien Phu

Kutoka Wikipedia, kamusi elezo huru
Picha ya wanajeshi wa Viet Minh wakipandisha bendera yao juu ya makao makuu ya Ufaransa yaliyotekwa huko Dien Bien Phu, Mei 7, 1954. Inasemekana picha hii inatokana na sinema ya Roman Karmen. Toleo la nakala isiyo na rangi.
Wafungwa wa kivita wa Kifaransa huko Dien Bien Phu mnamo 1954.

Vita ya Dien Bien Phu (pia; Mapigano ya Dien Bieb Phu) yalikuwa mapigano makubwa ya kivita yaliyotokea kati ya Novemba 1953 na Mei 1954 kati ya Viet Minh, vikosi vya ukombozi vya Vietnam vilivyoongozwa na Vo Nguyen Giap, na vikosi vya kikoloni vya Ufaransa. Vita hii ilikuwa mwarobaini wa kumaliza kwa utawala wa kikoloni wa Ufaransa huko Indochina na kuanzisha mgawanyiko wa Vietnam.

Dien Bien Phu ni bonde lililoko kaskazini-magharibi mwa Vietnam. Ufaransa iliamua kuweka kambi huko kwa lengo la kukata njia za usafirishaji za Viet Minh na kuvutia vikosi vyao katika mapigano ya moja kwa moja ambapo walihisi wangekuwa na faida kutokana na nguvu zao za kijeshi. Hata hivyo, wazo lao halikufua dafu mbele ya mbinu za kivita za Giap. Giap alipanga na kutekeleza mpango wa kukusanya maelfu ya wanajeshi na silaha kwa siri. Alifanya kazi usiku kucha na akitumia nguvu za wafanyakazi wa kawaida kuhamisha vifaa katika mazingira magumu ya milimani.

Mnamo tarehe 13 Machi 1954, Viet Minh walianza mashambulizi yao dhidi ya ngome za Ufaransa. Walitumia mbinu za kivita za msituni pamoja na silaha nzito kama mizinga na maroketi waliyoileta kwa mikono na baiskeli katika ardhi ya milimani. Vita vilianza kwa shambulio dhidi ya ngome za kando za Ufaransa, na kwa muda wa miezi miwili, Viet Minh walifanikisha kukamata ngome moja baada ya nyingine.

Vita ilifikia kilele chake tarehe 7 Mei 1954 wakati Viet Minh waliposhinda ngome kuu ya Ufaransa. Vikosi vya Ufaransa vilisalimu amri na askari zaidi ya 10,000 walikamatwa. Ushindi wa Dien Bien Phu ulikuwa na athari kubwa kwa Ufaransa. Ufaransa ililazimika kukubali kushindwa na kuanza mazungumzo ya amani ambayo yalifanyika Geneva.

Matokeo ya mazungumzo ya Geneva yalikuwa ni kugawanywa kwa Vietnam katika sehemu mbili: Vietnam Kaskazini chini ya utawala wa Kikomunisti ulioongozwa na Ho Chi Minh na Vietnam Kusini chini ya utawala wa mfalme Bao Dai na kisha serikali ya Ngo Dinh Diem iliyoungwa mkono na Marekani. Hii ilisababisha kuanza kwa migogoro mipya, Vita ya Vietnam, ambayo ilidumu hadi 1975.

  • Karnow, Stanley. Vietnam: A History. New York: Viking Press, 1983. ISBN: 978-0-670-74604-4.
  • Fall, Bernard B. Hell in a Very Small Place: The Siege of Dien Bien Phu. New York: Da Capo Press, 1967. ISBN: 978-0-306-80585-0.
  • Macdonald, Peter G. Giap: The Victor in Vietnam. New York: W. W. Norton & Company, 1993. ISBN: 978-0-393-03524-3.
  • Simpson, Howard R. Dien Bien Phu: The Epic Battle America Forgot. Washington, D.C.: Brassey's, 1994. ISBN: 978-0-02-881001-8.
  • Warren, James A. Giáp: The General Who Defeated America in Vietnam. New York: Palgrave Macmillan, 2013. ISBN: 978-1-137-27824-4.
  • Currey, Cecil B. Vo Nguyen Giap and the Vietnam War. New York: Franklin Watts, 1990. ISBN: 978-0-531-15136-1.
  • Moyar, Mark. Triumph Forsaken: The Vietnam War, 1954–1965. Cambridge: Cambridge University Press, 2006. ISBN: 978-0-521-85377-2.
  • Duiker, William J. Ho Chi Minh: A Life. New York: Hyperion, 2000. ISBN: 978-0-786-88325-3.
  • Lanning, Michael Lee, na Cragg, Dan. Inside the VC and the NVA: The Real Story of North Vietnam's Armed Forces. College Station: Texas A&M University Press, 1992. ISBN: 978-0-890-96299-9.
  • Tang, Truong Nhu. A Vietcong Memoir. New York: Vintage Books, 1985. ISBN: 978-0-394-74153-2.


Makala hii ni sehemu ya mradi wa kuboresha Wikipedia na Wikamusi ya Kiswahili. Unaweza kusaidia kuihariri na kuongeza habari.